MBUNGE UMMY ALIVYOPAMBANA KUZIRUDISHA KWENYE CHATI KLABU ZA COASTAL UNION NA AFRICAN SPORTS


Waziri
wa Afya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto Ummy Mwalimu  na
Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Tanga (CCM) kushoto akipokea tuzo ya
heshima kutoka kwenye Mwenyekiti wa Baraza la wazee la Klabu ya Coastal
Union ikiwa ni kutambua mchango wake kuisaidia timu hiyo wakati
ilipopanda daraja na kurudi Ligi kuu.


 Waziri
wa Afya Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto Ummy Mwalimu  na
Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Tanga (CCM)kulia akigawa vifaa vya
michezo kwa timu za soka mkoani Tanga zilizokuwa zikishirika Ligi ya
Banda Cup msimu uliopita ambapo vifaa hivyo alivitoa yeye.

WAZIRI
wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu na
Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Tanga katika akiwa na baadhi ya viongozi
wa timu ya Coastal Union wakati akipokwenda kuwakabidhi kiwanja eneo la
Maweni Jijini Tanga kushoto ni Mkurugenzi wa Jiji la Tanga Daudi Mayeji
kulia ni Mkurugenzi wa Kampuni ya City Plan Consultants (T) Limited Dkt
Juma Mohamed .


 Waziri
wa Afya,Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto  na Mbunge wa Viti
Maalumu Mkoa wa Tanga Ummy Mwalimu katikati akiwa na viongozi wengine
pamoja na timu ambazo alizikabidhi vifaa vya michezo jezi kwa ajili ya
kushiriki Mashindano ya Banda Cup msimu uliopita.


 Waziri
wa Afya,Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto  na Mbunge wa Viti
Maalumu Mkoa wa Tanga Ummy Mwalimu katikati akiwa na mashabiki wa timu
ya Coastal Union wakihamasisha ushindi wa timu ya Coastal Union kwenye
mechi zao za nyumbani katika Ligi Daraja la kwanza.



UNAPOZUNGUMZIA
mafanikio ya soka kwa Mkoa wa Tanga huwezi kuacha kulitaja jina la Ummy
Mwalimu ambaye ni Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa huo (CCM) na Waziri wa
Afya, Maendeleo ya Jamii Jinsia Wazee na Watoto ambaye amefanya kazi
kubwa kurudisha heshima ya michezo.

Sie sote ni mashahidi kwamba
bila juhudi kubwa ambazo alizifanya kwa kushirikiana na viongozi
wengine wa mkoa huo mkoani Morogoro wakati timu ya Coastal Union
ikitafuta tiketi ya kureja Ligi kuu ingekuwa ni ndoto wana Tanga
kushuhudia michuano hiyo mikubwa hapa nchini ikichezwa mkoani hapa.

Bila
kujali jambo lolote licha ya kuwa na shughuli za kitaifa alilazimika
kuungana na wana michezo mkoani Tanga kupiga kambi mkoani Morogoro ili
kuhakikisha anatimiza ndoto zake za kuhakikisha anaandika historia ya
kuirudisha Ligi kuu timu hiyo Kongwe hapa nchini ambayo ilishuka daraja
kabla ya kurejea tena.

Licha ya kuipandisha timu hiyo ikiwa
mkoani Morogoro lakini alilazimika kuisindikisha hadi mkoani Tanga akiwa
na msafara mkubwa wa magari huku akilakiwa na Mkuu wa Mkoa wa Tanga
Martine Shigella eneo la Pongwe huku akiendelea kuisapoti timu hiyo
katika Nyanja mbalimbali.

Hakuna asiyejua juhudi kubwa ambazo
amezifanywa kuhakikisha anapambana kwa hali na mali ili timu hiyo
inarudi Ligi kuu baada ya kushuka daraja mara kadhaa na kupoteza
mwelekeo ambapo aliamua kulivalia njuga suala hilo na kusimama kidete na
kufanikisha ndoto yake.

Katika makala hii leo Nataka japo
nikueleza jambo utambua kwamba unapomzungumzia Mbunge Ummy Mwalimu
amefanya nini kwenye kulipata mafanikio soka la Mkoa wa Tanga mpaka
limefikia hapo lilipo lakini pia ameendelea kuwa bega kwa bega na timu
kongwe za mkoa huo ambazo zilikuwa na historia ya soka.

Tukianzia
kwa Klabu ya Coastal Union “Wagosi wa Kaya” ambao mwaka 1988 waliandika
historia mkoani Tanga kwa kuchukua Ubingwa wa soka nchini ambao mpaka
sasa imekuwa ni klabu ambayo ikiingia katika kumbukumbu za mabingwa wa
nchi hii huwezi kuacha kuizungumzia.

Salimu Bawaziri ni Mjumbe
wa Kamati ya Mipango na Fedha katika timu ya Coastal Union anaeleza
kwamba mchango wa Mbunge Ummy ndani ya timu hiyo ni mkubwa na hauwezi
kusaulika kwani amekuwa mstari wa mbele kuwasaidia tokea wakiwa Ligi
daraja la kwanza mpaka akahakikisha timu inapanda daraja kwa
kushirikiana na viongozi.

“Nakumbuka wakati tukiwa kule mkoani
Morogoro tunapotafuta tiketi ya kupanda daraja mara kwa mara alikuwa
anakuja kukutana na wachezaji na viongozi kwa kutoa motisha na hamasa
kwa wachezaji kwa lengo la kuhakikisha tunapambana na kurejea Ligi kuu
hivyo mchango wake ni mkubwa sana mpaka tulipo sasa na bado amekuwa
akitusaidia”Anasema Bawaziri.

Anasema licha ya viongozi wengi
kusaidia lakini Mbunge Ummy aliweza kuibeba timu hiyo tokea kipindi timu
hiyo inashiriki Ligi daraja la kwanza hapa nchini na hakuweza kuiacha
pekee bali alikuwa akifika kambini kwa kuzungumza na wachezaji kuwapa
motisha jambo ambalo limechangia kwa asilimia kubwa kuweza kurudi ligi
kuu.

“Kwa kweli msaada ambao ametusaidia ni mkubwa na hatuwezi
kuusahau kufanya jitihada kubwa kwetu lakini pia kuweza kutusaidia
kuweza kupata uwanja eneo la Maweni lenye ukubwa wa mita 7632 mkubwa
ambao tutaanza kuufanyia kazi ambao huu utakuwa ni chachu kubwa kwa
maendeleo ya timu yetu”Anasema

Hata
hivyo anasema kuwa watahakikisha wanakuwa bega kwa bega naye kila
wakati kutokana na mchango wake mkubwa ndani ya timu hiyo na historia
ambayo ameiweka itakayodumu kwa vizazi na vizazi kwani kila
watakapotumia eneo hilo lazima watakumbuka jambo hili kubwa lilifanywa
na mbunge Ummy.

Hata hivyo Mbunge Ummy anaeleza dhamira yake ya
kusaka eneo hilo ambapo anasema kubwa zaidi ni kuisaidia timu hiyo
katika mipango iliyokuwa nayo kuanza kwenda vema huku wakijipanga kwa
hatua nyengine lakini kubwa kwa kuwa na eneo lake ambalo watalitumia
katika matumizi mbalimbali ikiwemo uwanja wa kuchezea.

““Nataka
niwaambie Coastal Union tutaendelea kuwa pamoja katika harakati zetu za
kuwania Ubingwa wa Ligi kuu labda niwahaidi kuwatafutia wadau pia
niwaambie bado tunaendelea kutafuta wadau na nihaidi hata ile block
yenye square mita 9600 yenye thamani milioni 48 nitafue wadau ili waweze
kupata eneo hilo”Anasema

Anasema atasaidia kutafuta wadau ili
kupata eneo hilo ambalo litakuwa kwa ajili ya matumizi ya ujenzi wa
Hosteli,Gym ya Mazoezi na Ukumbi wa sherehe wa Coastal Union kwa sababu
watu wa Tanga wana fanya sherehe na kitchen party kila siku

“Labda
ndugu zangu wapenzi wa soka na wana michezo wenzangu jambo hilo
limewezekana kutokana na mshikamano uliopo baina ya viongozi na
wanachama huku wakiwataka kuuendeleza ili kuweza kupata mafanikio
makubwa siku zijazo kwenye michuano ya ligi kuu”

Mbunge Ummy
hakuishia hapo lakini pia anasisitizia timu hiyo kufanya vizuri kwa timu
hiyo ndio imekuwa sababu ya kuwavuta wadau ambao wameweza kuwasaidia
katika masuala mbalimbali hivyo wachezaji na walimu wana kazi kubwa ya
kuhakikisha wanajipanga vema kwa ajili ya kufanya vizuri.

“Lakini
pia eneo hilo la kiwanja ambacho tuliwakabidhiwa timu hiyo nitagharamia
gharama za hati ya usajili mpaka kupata hati yenye jina la klabu ya
Coastal Union na hivi karibuni nitakwenda kuwakabidhi rasmi kwa lengo la
kuanza kuendelea na mipango yao “Anasema

Hata
hivyo Mbunge huyo anatoa wito kwa wakazi wa Jiji la Tanga wanaotaka
kuwekeza waende eneo la Pongwe ambalo lina viwanja 937 hivyo watumie
nafasi hiyo kwa sababu timu ya Coastal Union wakiwa hapo itavutia lakini
pia kuwepo kwa eneo kwa ajili ya zahanati kama walivyofanya kutoa kwa
shule ya Msingi.

Hatua ya Mbunge Ummy kuikabidhi eneo timu hiyo
kulipelekea Mwenyekiti wa Coastal Union Steven Mnguto kuishiwa na maneno
ya kuzungumza huku akionyesha furaha yake isiyokuwa ya kifani kwake kwa
kuisaidia timu hiyo lakini pia kuweza kurudisha heshima ya soka kwa
mkoa huo.

“Mh Mbunge hapa nilipo nimeishiwa maneno ila nisema
mama Ummy umetusaidia sana ulikuwa wapi siku zote kauli ya Mungu anasema
nitakuwa muda na saa usizotarajia kila tunapofanyaa tukio kubwaa
tunaona nyota inatuandama tulipata basi wakati tunapanda daraja kipindi
kile safari hii tumepanda nyota nyengine imekuja kiwanja tuendelee
kuomba na kushikamana”Anasema.

Hata hivyo naye Mwenyekiti wa
Chama cha Soka Mkoa wa Tanga (TRFA) Saidi Soud anasema wao kama
wasimamizi wa soka la mkoa wa Tanga wamehemewa na furaha kwa jambo hilo
ambalo ni la kihistoria kutokana namna Waziri huyo alivyowashika mkono.

“Labda
nisema Waziri Ummy ni mama wa kweli nakumbuka wakati unasema utatushika
mkono huko mbele tulikuwa tunasuasua lakini ujio wako umesaidia kuvunja
hata makundi yaliyokuwa yakirudisha nyuma maendeleo “Anasema.

Akizungumza
katika Halfa hiyo, Mkurugenzi wa Kampuni ya City Plan Consultants (T)
Limited Dkt Juma Mohamed anaeleza namna Mbunge Ummy alivyofanikisha
upatikanaji wa eneo hilo ambapo anaeleza kwamba walipata ombi kutoka
kwake na kuona namna ya kupata eneo la Michezo kwa timu ya Coastal
Union.

Anasema baade waliweza kulijadili na kuliwasilisha kwa
wadau ambao ni wananchi wa eneo la hapa na kuweza kupatikana kwa eneo
hilo ambapo pia unaweza kutoa viwanja cha mpira hamsini kwa mia moja
lakini panazaidi ya eneo la pitch ya mpira.

“Tulikubaliana
kuhifadhi viwanja 16 upande block za chini kwani kuna masuala
wanaendelea na majadiliano vitalipiwa kwa ajili ya kuweka maeneo
mbalimbali ya michezo nah ii itafungua ukurasa mpya wa soka kwa mkoa
“Anasema Dkt Juma.

Licha ya hivyo Mbunge Ummy aliweza kufanya
ziara ya mara kwa mara kutetembelea kambi ya timu ya Coastal Union
iliyokuwepo eneo la Saruji Jijini Tanga wakati timu hiyo ikishiriki
daraja la kwanza na nikiwa kwenye nafasi ya tatu kwenye kundi B.

Baada
ya kutembelea kambi hiyo aliwasisitizia wachezaji kuongeza jitihada na
kujituma ili kushinda mechi nne zilizobakia kwa lengo la kujihakikishia
nafasi ya kucheza ligi kuu ya Tanzania bara msimu wa mwaka 2018/2019
jambo ambalo lilifanikiwa na kuiwezesha timu kurudi ligi za juu.

“Katika
nukuu ya maneno yake wakati huo ndugu zangu “Coastal Union ikipanda
daraja na kucheza Premier League sio tu itawezesha vijana kupata kipato
bali pia itachochea uchumi na maendeleo ya Jiji la Tanga mwisho wa
kunukuu“

Katika kuhamasisha huko Mbunge Ummy aliwakabidhi
shilingi milioni 3 na nusu kwa ajili ya mishahara ya wachezaji ya mwezi
Desemba na gharama za chakula huku akihaidi kutoa zawadi y ash.milioni 2
kwa kila mechi watakayoshinda kati ya mechi nne zilizobaki.

Baada
ya hatua hiyo Kocha Mkuu wa timu ya Coastal Union Juma Mgunda
amemuhakikishia Mbunge Ummy kuwa vijana wapo tayari kufanya vizuri
kwenye Ligi na hivyo hatutakuangusha katika michezo yao hiyo iliyosalia
katika michuano ya Ligi Daraja la kwanza jambo ambalo walilfanikisha kwa
asilimia kubwa na kurejea ligi kuu.

Pia walimshukuru Mbunge
Ummy kwa kujitoa kwake ili kuhakikisha timu hiyo inapanda daraja ambapo
tukio hilo la makabidhiano limehudhuriwa na Mwenyekiti wa Chama cha
Mpira wa Miguu mkoa wa Tanga (TRFA) Said Soud na Mjumbe wa Kamati ya
Utendaji ya Coastal Union Salim Bawaziri

“Motisha kwa wachezaji wa timu ya Coastal Union”

Mbunge
Ummy kwa kuonyesha kujali na kuwathamini wana michezo mkoani Tanga
alilazimika kuwalipa wachezaji wa timu ya Coastal Union na African
Sports mishahara kwa kipindi Fulani huku akihamasisha uwanjani.

Hatua
hiyo inatajwa kwamba imechangia uwepo wa timu hiyo kwenye Ligi madaraja
tofauti huku zikiendelea kufanya vizuri kutokana na uwepo wake ambao
umekuwa na mchango mkubwa kwenye soka.

Wakati mwengine wana
Tanga ambao wanakuwa wakijitokeza kwenye viwanja vya Mkwakwani
wametakuwa ni mashahidi tosha Mbunge Ummy amekuwa akihudhuria mechi za
timu hiyo licha ya kuwa nje ya mkoa huo kwa wakati huo lakini hulazimika
kufika hata kipindi cha pili uwanjani ikiwa ni kuwahamasisha
wanamichezo.

Kutembelea kambi ya wachezaji.

Ummy ni
miongoni mwa viongozi wachache ambao kila wakati timu ya Coastal Union
inapojiandaa kwa ajili ya kucheza na timu kubwa nchini ikiwemo Simba,
Yanga na hata nyengine amekuwa akitinga kambini kuzungumza na wachezaji
ikiwezekana kula nao chakula cha mchana huku akiwahamasisha suala la
ushindi ni lazima.

Hatua hiyo imetajwa kwamba imechangia kwa
asilimia kubwa wachezaji wa timu hiyo kupata hari kubwa ya kuweza
kufanya vizuri katika michuano ya Ligi Daraja la kwanza na hatimaye
kurudi Ligi kuu na kudumu mpaka wakati huo.

Uhamasishaji.

Mbunge
Ummy ambaye siku zote nimeshindwa nimfananishe na kiongozi gani hapa
nchini amekuwa na desturi ya kila mechi zinapokuwa zikicheza timu kongwe
za mkoa wa Tanga amekuwa akishirikiana na mashabiki na wapezi
majukwaani kuhamaisha ushindi kwa staili ya kushangilia.

Staili
hiyo ya ushangiliaji ilipelekea kuchangia kuwaibua mashabiki wengi wapya
ndani ya timu hiyo ambao kila timu hiyo inapokuwa ikicheza mechi zake
za nyumbani wanalazimika kufika uwanjani na kuujaza uwanja hali ambayo
ilichangia kwa asilimia kubwa kwenye michezo ya nyumbani timu kufanya
vizuri kutokana na hamasa.

Hata hivyo Mbunge Ummy hakuiacha
nyuma Klabu ya African Sports ambao waliwahi kuwa mabingwa wa kombe la
Muungano mwaka 1988 ambapo wakati huo taji hilo ndio lilikuwa kubwa
zaidi nchini,michuano hiyo iliyoshirikisha timu za Bara na Visiwani na
kumpata bingwa wa jumla wa nchi na pia wawakilishi wa michuano ya
Afrika.

Bingwa wa Bara alikuwa anakwenda kucheza Klabu Bingwa
Afrika Mashariki na Kati pekee,lakini bingwa wa Muungano wakati huo
alikuwa anacheza Klabu Bingwa Afrika na mshindi wa pili wa Ligi ya
Muungano, alikuwa anacheza iliyokuwa michuano ya Kombe la Washindi
Afrika, baadaye ikaongezeka na mshindi wa tatu akawa anacheza Kombe la
CAF.

Pamoja na kushiriki michuano hiyo lakini miaka ya nyuma
timu hiyo iliyumba na kushuka daraja kwa nyakati tofauti licha ya
kurejea Ligi kuu lakini ilishindwa kuhimili mikimikii ya ligi hiyo na
kujikuta wakishuka daraja wao na mahasimu wao Coastal Union na Mgambo
Shooting kwa wakati mmoja.

Baada ya kushuka daraja wakajikuta
wakishindwa kuhimili vishindo vya daraja la kwanza na kujikuta wakirudi
kucheza Ligi daraja la pili walilopo mpaka wakati huu huku wakipambana
kuhakikisha wanarejea walipotoka kwa kuweka mipango imara ambayo
itawafikisha huko.

Kwa kuona hali ya timu hiyo Mbunge Ummy
aliamua kujitosa na kuanza kuisaidia katika masuala mbalimbali ikiwemo
vifaa vya vyenye thamani ya zaidi ya milioni 1.5 ikiwemo vyakula wakati
wa kamb na motisha ikiwa ni mkakati kabambe wa kuhakikisha timu hiyo
inafanya vizuri kwenye mashindano wanayoshiriki na hatimaye kucheza ligi
daraja la kwanza msimu ujao.

Mbunge Ummy anasema vifaa hivyo
vitakuwa ni chachu ya timu hiyo kuweza kufikia malengo yao huku akieleza
dhamira yake kubwa ni kuhakikisha timu hiyo inarejea ligi daraja la
kwanza na ile ya Coastal Union ihakikisha msimu ujao inarudi Ligi kuu.

“Niseme
tu sisi tumejipanga kuhakikisha tunazirejesha timu hizi kwenye michuano
ya Ligi kuu soka Tanzania bara tukianzia na timu ya Coastal Union
lakini ndugu zangu African Sports mhakikishe mnarudi ligi daraja la
kqwanza na baadae ligi kuu “Anasema

Akizungumza baada ya kupokea
vifaa hivyo, Mwenyekiti wa Klabu ya African Sports, Awadhi Salehe Pamba
anamshukuru Waziri Ummy kwa kuwasaidia msaada huo ambao utakuwa ni
chachu kwao kuweza kufikia malengo yao kutokana na changamoto hiyo
kwisha.

Alisema msaada uliotolewa na Mbunge Ummy utakuwa chachu
kubwa kwao kuweza kufikia malengo yao waliojiwekea ya kuhakikisha
wanarudi ligi kuu kwani ndio ndoto yao kubwa ambayo wamekuwa wakiiwaza
kila wakati.

“Mbunge Ummy tukushukuru sana katika hili umetupa
nguvu ya kuweza kupambana na tuna kuhaidia kuhakikisha tunairudisha timu
Ligi daraja la kwanza na hatimaye ligi kuu.

Comments