Muungano wa G7 na Umoja wa mataifa walaani mapigano mapya Libya

Vikosi tiifu kwa serikali ya Tripoli vikisaidia kulinda mji mkuu, April 2019
Vikosi tiifu kwa serikali ya Tripoli vimeripotiwa kuungana na serikali kulinda mji mkuu

Mataifa yenye uwezo mkubwa wa kiuchumi duniani G7, pamoja na Umoja wa mataifa yamelaani vikali mapigano yaliozuka upya nchini Libya.

Mataifa hayo yanataka pande zinazohasimiana Libya "kusitisha mara moja shughuli za kijeshi". Baraza kuu la Usalama la Umoja wa Mataifa pia limetoa wito huo.

Tripoli ni makao makuu ya serikali ya Libya inayotambuliwa kimataifa, na ambayo pia inaungwa mkono na Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa.

Vikosi vya kulinda usalama vya umoja wa mataifa katika mji huo vimekuwa katika hali ya tahadhari.

Ghasia zimekumba Libya tangu utawala kiongozi wa nchi hiyo wa mda mrefu, Muammar Gaddafi kuangushwa na yeye kuuawa mwaka 2011.

Nini kinachofanyika?

Kamanda Khalifa Haftar, ambaye ni kiongozi wa vikosi vya kijeshi vinavyopinga utawala wa Tripoli siku ya Alhamisi aliamuru vikosi vyake kuingia mji wa Libya.

Hatua hiyo ilijiri wakati Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres, akiwa mjini humo kujadili mzozo unaoendelea sasa.

Kumeripotiwa mapigano karibu na uwanja wa kimataifa wa ndege uliyopo kusini mwa mji huo.

Jenerali Haftar alikuzungumza na Bw. Guterres mjini Benghazi siku ya Ijumaa, na inaripotiwa kuwa alimwambia kiongozi huyo kuwa oparesheni yake haitakomeshwa hadi pale vikosi vyake vitakaposhinda "ugaidi".

Jenerali Haftar
Kamanda wa jeshi Khalifa Haftar awaamuru wanajeshi kuandamana na kuingia Tripoli

Siku ya Alhamisi, vikosi vya jeshi la kitaifa la Libya LNA, vinavyopinga utawala wa Tripoli vilitwaa udhibitwa wa mji wa Gharyan uliyoko kilo mitta 100 kusimi mwa Tripoli.

Pia kumeripotiwa kuwa vikosi hivyo vimedai kuteka uwanja wa ndege wa kimataifa mjini Tripoli ambao ulifungwa tangu mwaka 2014 - japo madai hayo yamekanushwa.

Wakaazi wa Misrata mashariki mwa Tripoli wameliambia shirika la habari Reuters kuwa wanamgambo katika mji huo wameagizwa kuenda kuulinda mji wa mkuu.

Makundi yaliyojihami yanayoonga mkondo serikali ya Tripoli wameimbia Reuters siku ya Ijumaa kuwa wamewakamata wapiganaji kadhaa wa LNA.

Vikosi vya LNA vilitwaa udhibiti wa maeneo ya kusini mwa Libya na visima vyote vya mafuta katika maeneo hayo tangu mwazo wa mwaka huu.

Mapigano haya mapya yamepokelewaje?

Katika mtandao wake wa Twitter, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres, aliandika kuwa ameondoka Libya akiwa na ''hofu na masikitiko makubwa'' lakini ana matumaini kuwa ufumbuzi wa mzozo unaoendelea utapatikana ili kuzuia mapigano katika mji mkuu wa Tripoli.
map

Baadae Muungano wa G7 ulijibu kw kutoa wito kwa pande zinazozozana kusitisha mapigano mara moja.

"Tunapinga kwa kauli moja hatua za kijeshi nchini Libya," ilisema taarifa ya muungano huo, huku ikisisitiza kuwa inaunga mkono juhudi za Umoja wa Mataifa wa kusaidia taifa hilo na kutoa wito kwa jamii ya kimataifa kushirikiana kufikia hatua hiyo.

Khalifa Haftar ni nani?

Haftar ni afisa wa kijeshi wa zamani aliyemsaidia kanali Muammar Gaddafi kuingia madarakani mwaka 1969 kabla ya kutofautiana na kiongozi huyo na hatimaye kukimbilia mafichoni nchini Marekani.

Alirejea nchini Libya mwaka 2011 baada ya maandamano ya kupinga utawala wa Gaddafi kuanza na kuwa kamanda wa waasi.

Mwezi Disemba mwaka jana Haftar alikutana na Waziri mkuu Fayez al-Serraj wa serikali inayoungwa mkono na Umoja wa Mataifa lakini alikataa kuhudhuria mkutano rasmi na kufanya mazungumzo na yeye.

Wiki iliyopita alizuru Saudi Arabia, ambako alikutana na Mfalme Salman na mwana mfalme Mohammed bin Salman na kufanya mazungumzo nao.

Comments