Alichosema Mimi Mars kuhusu kuhamia kwenye Gospel pamoja na Vanessa

Msanii wa Bongo Flava kutoka Mdee Music, Mimi Mars amefunguka iwapo yeye na Vanessa Mdee kuna siku wataingia rasmi katika muziki wa Injili.
Utakumbuka Mimi Mars pamoja na Vanessa Mdee wameshirikishwa na dada yao, Nancy Hebron ambaye anafanya muziki wa Injili katika wimbo wake uitwao Beauty Jesus.

Muimbaji huyo amesema kuwa walishiriki katika wimbo huo kwani waliombwa kufanya hivyo ila haimanishi kuwa wana mpango wa kuingia huko moja kwa moja.

“Hapana, Nancy ni mtu ambaye ni ndugu yetu na ameingia kwenye muziki hivi karibuni na aliomba sana tufanye naye wimbo wa gospel, kwa hiyo tukaona si vibaya ingawa tunafanya muziki wa dunia pia tunamwabudu Mungu, tunaenda kanisani,” amesema.

“Sio kwamba namaanisha tunaingia kule, hapana!, lakini ilikuwa ni kum-support na kuonyesha watu tupo hata kwenye suala la dini,” ameongeza.

Tangu kuingia kwake rasmi kwenye Bongo Flava mwaka jana na kuachana na kazi ya utangazaji, Mimi Mars ameweza kutoa nyimbo nne ambazo ni Sugar, Dede, Sitamani, Papara pamoja na kufanya kolabo kadhaa.

Comments