Watumishi 134 wa hospitali ya Muhimbili waligushi vyeti

Hospitali ya taifa ya Muhimbili nchini Tanzania
Hospitali ya taifa ya Muhimbili nchini Tanzania
               
Watumishi 134 wa hospitali ya taifa Muhimbili wamebainika kuwa na vyeti vya kughushi vya ngazi ya elimu ya sekondari Tanzania.
Taarifa kutoka kwenye uongozi wa hospitali hiyo imesema , hospitali iliendesha zoezi la uhakiki wa vyeti vya elimu vya sekondari kwa watumishi wake kwa kushirikiana na baraza la mitihani la Tanzania (NECTA) baada ya agizo la serikali kutaka uhakiki ufanyike kwa watumishi wa Umma.
Idara iliyoathirika zaidi ni idara ya uuguzi ambapo watumishi wake takriban 70 wamekutwa na vyeti vya kughushi.
Baadhi ya idara nyingine zilizoguswa kwenye zoezi hilo ni idara ya tiba watumishi 20, tiba shirikishi watumishi 14, upasuaji watumishi wanne, idara ya Tehama watumishi 11, rasilimali, ufundi, fedha na mipango.

Kutokana na dosari hizo, uongozi huo umesema watumishi waliobainika wamekosa sifa za kuendelea kuwa watumishi wa umma hivyo wametakiwa kujiondoa wenyewe kazini kabla ya tarehe 15 mwezi Mei mwaka 2017 ili kuepuka kuchukuliwa hatua za kisheria.
Uongozi wa Muhimbili umetoa orodha ya watumishi walioghushi vyeti na kuwataka wakuu wa Idara mbalimbali kuhakikisha kuwa wafanyakazi wanaohusika hawaendelei kutoa huduma hospitalini hapo.
Mwezi Aprili mwaka huu Rais wa Tanzania Dokta John Pombe Magufuli alipokea ripoti ya uhakiki wa watumishi wa Umma mjini Dodoma na kuagiza watumishi waliobainika kughushi vyeti wakatwe mishahara ya mwezi Aprili na kuamuru watumishi ambao watakuwa hawajaondoka mahali pa kazi wakamatwe na kufikishwa mahakamani, ambapo ikiwa watabainika kutenda kosa hilo watahukumiwa kifungo cha miaka saba gerezani.

Comments