Serikali ya Kenya yapunguza bei ya unga wa mahindi


Bidhaa mbalimbali za unga
Wakenya wameghadhabishwa na bei ya unga iliyoongezeka kwa muda
Imekuwa ni afueni kwa Wakenya baada ya serikali kutangaza kupunguzwa kwa bei ya unga na kuondoa ushuru unaotozwa kwa bidhaa kama vile maziwa na sukari.
Kwenye kikao na waandishi mjini Nairobi, Waziri wa kilimo nchini humo, Willy Bett ameiondolea serikali lawama za ongezeko la bei ya unga nchini Kenya.
Kwa wiki kadhaa sasa, raia wa taifa hilo wamekuwa wakishuhudia ongezeko la bei ya unga na bidhaa nyingine muhimu huku raia wakiilaumu serikali.
Kuanzia Jumatano, raia sasa watanunua kilo moja ya Unga kwa shilingi 47 za Kenya sawa na nusu dola ya Marekani kutoka shilingi 100 za Kenya au dola moja.
 
Waziri Bett ameeleza kuwa serikali inashirikiana na kampuni za unga kutathmini bei ili kurahisisha gharama za bidhaa hiyo muhimu kwa raia.
Hata hivyo, Waziri huyo amefafanua kuwa hali hiyo imesabababishwa na ukame uliokithiri na kupelekea uhaba wa zao hilo.
Bei ya gunia la kilo 90 za mahindi lililokuwa likinunuliwa kwa dola 23 za Marekani lilikuwa limepanda bei na kufikia dola 46.
Kwenye mkataba kati ya serikali na waingizaji na wasambazaji wa unga, gunia moja litauzwa kwa dola 23 huku bei hiyo ikitarajiwa kuanza rasmi Jumatano.
Waziri Bett amepinga kuhusika kwa serikali katika uingizaji wa unga na kuongeza kuwa kazi yake ni kuwaondolea waingizaji ushuru unaotozwa kuingiza bidhaa hiyo. Serikali ya Kenya inalenga kuingiza mifuko milioni 5 ya mahindi kutoka mataifa ya Zambia na Ethiopia.

Comments