Magufulia aivunja mamlaka ya ustawishaji wa makao makuu Dodoma

Magufuli amesema majukumu yote ya CDA yatahamishiwa Manispaa ya Dodoma
Magufuli amesema majukumu yote ya CDA yatahamishiwa Manispaa ya Dodoma
               
Rais wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli ameivunja rasmi Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu Dodoma (CDA) na kuagiza mali na shughuli zote zilizokuwa zikifanywa na CDA zihamishiwe Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma.
Rais Magufuli amesema ameamua kuivunja CDA na kuhamishia majukumu yake katika Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma ili kuondoa mkanganyiko wa utoaji wa huduma kwa wananchi.
Amesema mkatanganyiko huo ulikuwa ukisababishwa na mgongano kati ya vyombo hivyo viwili.
Aidha, amesema mahitaji ya sasa yamedhihirisha kuwa hakuna haja ya kuwepo kwa CDA.
"Wananchi wa Dodoma wamelalamikia tatizo hili kwa muda mrefu sana, hata nilipokuwa kwenye kampeni zangu za uchaguzi mkuu wa mwaka 2015 walilalamika sana, sasa nimetekeleza niliyowaahidi," amesema Dkt Magufuli.
"Naamini kwa uamuzi huu malalamiko ya wananchi yatapata utatuzi na pia tutakuwa tumeondoa kikwazo cha umiliki wa muda mfupi wa ardhi uliosababisha wawekezaji kushindwa kujenga viwanda Dodoma.
"Sasa majukumu yote yanahamishiwa Manispaa ya Dodoma, sitaki kuendelea kusikia visingizio, mkajipange mambo yaende vizuri."
Rais Magufuli ameivunja CDA kwa kutia saini hati ya Amri ya Rais ya kuivunja Mamlaka hiyo katika ikulu jijini Dar es Salaam.
Aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa CDA Mhandisi Paskasi Muragili atapangiwa kazi nyingine na Dkt Magufuli ameagiza wafanyakazi wote wa Mamlaka hiyo wahamishiwe Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma na ofisi nyingine za Serikali kadiri inavyofaa.
Aidha, kiongozi huyo ameagiza hati zote za kumiliki ardhi zilizokuwa zikitolewa na CDA kwa ukomo wa umiliki wa miaka 33 zibadilishwe na kufikia ukomo wa umiliki wa miaka 99 kama ilivyo katika maeneo mengine nchini ili kuwavutia wawekezaji hasa wa viwanda.
Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu Dodoma (CDA) ilianzishwa kwa Amri ya Rais ya tarehe 01 Aprili, 1973 na kutangazwa kupitia tangazo la Serikali namba 230.

Comments