Arusha: Majonzi Ibada ya Kuaga Wanafunzi 32 wa Lucky Vicent Waliofariki Ajalini

Mmoja wa waliohudhuria ibada hiyo akifarijiwa
Mmoja wa wazazi waliohudhuria ibada hiyo akifarijiwa
               
Mamia ya watu wamejitokeza kuhudhuria ibada ya pamoja kuwaaga wanafunzi 32 wa shule ya Lucky Vicent waliofariki dunia ajalini Jumamosi asubuhi.
Mwandishi wa BBC aliyepo Arusha Aboubakar Famau anasema majeneza yenye miili ya waliofariki tayari imefikishwa na kupangwa katika meza maalumu ambapo sala maalumu itafanyika ili kutoa heshima ya mwisho.
 
Mpaka sasa uwanja wa Sheikh Amri Abeid umejaa mamia ya wakaazi wa mkoani Arusha huku wengine wakitoka maeneo mbalimbali.
Baadhi ya watu waliokuja kuomboleza wamepoteza fahamu hivyo kupewa huduma ya kwanza huku wengine wakikimbizwa hospitalini.
Makamu wa rais Bi Samia Suluhu Hassan ni miongoni mwa viongozi wakuu serikali wanahudhuria ibada hiyo.
Amevitaka vyombo husika vihakikishe suala la usalama barabarani linapewa kipaumbele.
"Nawaasa madereva kuwa makini wawapo barabarani na serikali itaendelea kuboresha miundombinu ya barabara," amesema.
Waziri wa elimu wa Kenya Dkt Fred Matiang'i, mmoja wa wageni kutoka nje ya Tanzania waliohudhuria ibada hiyo, amewapa pole Watanzania kwa msiba huo.
"Kenya itaendelea kuwa pamoja nanyi kwenye kipindi hiki kizito cha msiba huu mzito uliowafika. Msiba huu si wa Tanzania peke yake ni wa wote hata kwetu Kenya Rais Kenyatta na mkewe wanawapa pole sana na kuwaombea," amesema.
Majenza yakitolewa kwenye lori
Majeneza yakitolewa kwenye lori na wanajeshi wa JWTZ
Wanafunzi hao wa darasa la saba walifariki dunia pamoja na walimu 2 na dereva wa gari la shule hiyo ya msingi ya Arusha baada ya gari walilokuwa wakisafiria kupata ajali katika eneo Rhotia Marera, Wilaya ya Karatu Mkoani Arusha.
Wanafunzi na walimu hao walikuwa wakitoka shuleni kwao kwenda shule ya msingi iitwayo Tumaini kwa ajili ya kufanya mtihani wa ujirani mwema na walipofika katika eneo la Rhotia Marera basi walilopanda liliacha njia na kisha kutumbukia korongoni.
Wanafunzi watatu walijeruhiwa.
Rais Magufuli, akituma salamu za rambirambi Jumamosi alisema „ajali hiyo imezima ndoto za watoto waliokuwa wakijiandaa kulitumikia taifa na imesababisha uchungu, huzuni na masikitiko makubwa kwa familia za marehemu na Taifa kwa ujumla."
"Muhimu kwa sasa tuwaombee marehemu wote wapumzishwe mahali pema, majeruhi wapone haraka na wote walioguswa na msiba huu wawe na moyo wa subira, ustahimilivu na uvumilivu katika kipindi hiki kigumu."
Baadhi ya waliohudhuria ibada hiyo wamezidiwa na huzuni
Baadhi ya waliohudhuria ibada hiyo wamezidiwa na huzuni
Manejewa yakiwa kwenye meza maalum
Majeneza yakiwa kwenye meza maalum
Wakazi wamejitokeza kwa wingi
Wakazi wamejitokeza kwa wingi

Comments