MAYANGA: NITAIPELEKA STARS 'AFCON 2019

Baada ya Shirikisho la soka Tanzania TFF, kumtangaza kocha wa Mtibwa Sugar Salum Mayanga, kuwa kocha mkuu wa timu ya taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ kocha huyo amesema yupo tayari kwa kazi hiyo na kuwataka wadau mbalimbali wa mchezo huo kumpa sapoti ili kufanikisha adhamira yake ya kuifikisha mbali timu hiyo.

Mayanga ameongea na mtandao wa Goal amesema, ameupokea kwa mikono miwili uteuzi huo ingawa ni kazi ngumu na yenye kuhitaji ushirikiano wa watu wengi, lakini atajitahidi kuhakikisha mambo yanakwenda sawa na timu ya taifa kufanya vizuri katika michuano ambayo inaikabili.

“Kuwa kocha wa timu ya taifa siyo kitu cha mchezo kwasababu kuna vitu vingi hasa ukizingatia timu hii kila mtu anasauti nayo kwahiyo nawaomba wadau tushikamane na kupeana sapoti ili kila tutakacho kifanya iwe ni kwa umoja wetu na mafanufaa ya wote,”amesema Mayanga.

Kocha huyo amesema jukumu lake kubwa ni kuhakikisha anakuwa makini katika kuwafatilia wachezaji na kuteua kikosi ambacho kitakubalika na Watanzania wote ili pindi timu inapopata matokeo mabaya watu wasimtupie lawama kocha.

Kocha huyo ameelezea mikakati yake ya kujenga timu imara ambayo itawashirikisha wachezaji wote wanaofanya vizuri kwenye klabu zao za ndani na nje ya Tanzania.

“Niwaombe wachezaji wazingatie na kulinda viwango vyao tunajenga timu yetu sote hivyo nilazima kwanza tuwe na uchungu nao na tuweke wivu wa mafanikio, kwani hatuwezi kuwaona Uganda wanakwenda kushiriki AFCN, na sisi tupo tukiwaangalia,” amesema Mayanga.

Kocha huyo amesema ataendeleza mikakati ya kocha aliyepita Boniface Mkwasa ambaye alikuwa akisisitiza nidhamu na uwanjibikaji wa kila mchezaji kwenye timu yake hivyo hatomuita mchezaji kwenye kikosi chake kutokana na jina lake au umaarufu aliokuwa nao.

Mayanga anachukua nafasi ya Mkwasa ambaye amemaliza mkataba wake wa mwaka mmoja kuifundisha timu hiyo akiwa kama kocha mzawa, akichukua mikoba ya Mholanzi Mart Nooij, ambaye alikatishiwa mkataba wake kutokana na mwenendo mbaya wa timu hiyo.

Source: Goal.com

Comments