HIZI NDO STORI ZA MAGAZETI YA LEO

MWANANCHI
Watu watano wamefariki dunia kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha jijini Dar es Salaam, watatu kati yao wakiwamo wanafunzi wawili, wakipoteza maisha baada ya kibanda walichojihifadhi kujikinga na mvua kuangukiwa na nguzo ya umeme na kuwaunguza.
Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa kipolisi wa Temeke, Zakaria Sebastian alisema vifo vya watu hao watatu vilitokea katika eneo la Mchikichini Kimbangulile, Mbagala.
Sebastian aliwataja waliokufa kuwa ni Ramadhan Said (10), mwanafunzi wa darasa la nne Shule ya Msingi Mchikichini, Alhaji Jumanne (15), mwanafunzi wa kidato cha kwanza Shule ya Sekondari ya Charambe na Monica Elistone (26).
Alisema wakati mvua ikiendelea kunyesha, watu hao walijihifadhi kwenye kibanda kilichotengenezwa kwa mabati na ghafla waya wa nguzo hiyo ulikatika na kuangukia kibanda hicho na kushika moto.
“Wakiwa kwenye banda hilo, ghafla nguzo ilianguka na waya wake kuangukia kibanda kilichoshika moto na kuwateketeza watu hao,” alisema  Kamanda Sebastian.
Mjumbe wa shina namba nne wa mtaa huo, Kondo Namna alisema zaidi ya  nguzo saba zimeinamia kwenye nyumba za watu na wameshatoa taarifa Tanesco, lakini hadi jana, hakuna hatua zozote zilizochukuliwa na shirika hilo.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, Camillius Wambura alisema wakati mvua zinaendelea kunyesha saa sita usiku wa kuamkia jana, mkazi wa Mwananyamala Edward Warioba (22) alifariki dunia baada ya kuangukiwa na ukuta akiwa amelala nyumbani kwake.
Katika tukio jingine, Kamanda Wambura alisema maiti ya mwanamume mwenye umri wa kati ya miaka 45 na 50 iliokotwa ikielea kwenye makutano ya Mto Goba na Makongo.
Alisema huenda mtu huyo alisombwa na maji ya mvua katika eneo ambalo bado halijajulikana. Wakati maafa hayo yakitokea, Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), imetoa tahadhari ya kuwapo kwa mvua kubwa katika maeneo ya ukanda wa Pwani na kuwataka wakazi wa maeneo hayo kuwa makini.
MWANANCHI
 Marais wa nchi sita za Afrika kesho watakuwa na mkutano mkubwa jijini hapa, juu ya uwekezaji na uboreshaji katika ukanda wa kati huku wakitarajiwa kujadili changamoto za kadhaa za kiuwekezaji.
Marais hao ni Joseph Kabila wa Jamhuri ya Demokrasia ya Kongo (DRC), Pierre Nkurunziza wa Burundi, Paul Kagame wa Rwanda, Yoweri Museveni wa Uganda, Uhuru Kenyatta wa Kenya na mwenyeji wao wa Tanzania, Rais Jakaya Kikwete.
Mkutano huo wa siku mbili utaambatana na mdahalo baina ya viongozi hao na wadau mbalimbali wa maendeleo.
Mjadala wa viongozi hao utajikita katika umuhimu wa ukanda wa kati ambao ni kiungo muhimu katika ukuaji uchumi wa nchi hizo kwa kuwa husaidia katika uingizaji na uuzaji wa bidhaa mbalimbali kupitia Tanzania kwa njia za maji, reli na barabara.
Nchi hizo zimekuwa zikiathiriwa na gharama kubwa za uendeshaji biashara ambazo zinahusiana na bei kubwa ya usafirishaji, vikwazo vya kibiashara, ucheleweshaji na gharama lukuki za kiutawala zinazobadilika mara kwa mara.
Wakati wa mkutano huo, viongozi hao watafanya uzinduzi wa treni ya mizigo kuelekea Uganda, Rwanda na DRC.
Mkutano huo utafanyika majuma kadhaa baada ya ule wa Ukanda wa Kaskazini kufanyika jijini Kigali, Rwanda, ambao Rais Kikwete alialikwa na kuweka hisia tofauti kuwa huenda kuna mashindano baina ya kanda hizo mbili. Nchi za Rwanda, Uganda, Burundi, DRC pia ni wadau wa ukanda wa Kaskazini.
Ripoti ya ufuatiliaji maendeleo ya ukanda huo kwa mwaka 2013 iliyotolewa na Wakala wa Kuwezesha Biashara na Usafirishaji katika Ukanda wa Kati (CCTFA), ilibainisha kuwapo mizani saba na vituo tisa vya ukaguzi vinavyochelewesha biashara.
Ripoti hiyo ilibainisha kuwa uingizaji wa mizigo kupitia Bandari ya Dar es Salaam uliongezeka hadi tani bilioni 11.3 mwaka 2013 kutoka tani bilioni 4.95 mwaka 2013 huku DRC ikiongoza kupitisha mizigo yake baada ya mwenyeji, Tanzania.
Kama zilivyo nchi wanachama wa ukanda huo, Tanzania imejiwekea malengo lukuki ya kuboresha ukanda wa kati hususan reli ya kati baada ya kuifanya kuwa moja ya vipaumbele sita vya Mpango wa Matokeo Makubwa Sasa (BRN).
Baadhi ya wadau walisema Tanzania haitakiwi kukata tamaa kutokana na changamoto inazokabiliana nazo katika kutekeleza miradi ya ukanda wakati kwa manufaa yake na nchi jirani.
MTANZANIA
Aliyekuwa Mbunge wa Kigoma Kaskazini kwa tiketi ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Zitto Kabwe, amesema atafanya kazi kukijenga chama Alliance for Change and Transparency (ACT-Tanzania) kwa kukipaisha kama alivyofanya kazi akiwa ndani ya Chadema.
Amesema akiwa kiongozi Chadema kwa miaka zaidi ya 20 alifanya kazi ya kukijenga chama na kuhakikisha kinatoka kuwa na wabunge wanne na sasa kimepanda na kuwa na wabunge 48.
Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Zitto alizitaja sababu tano zilizomfanya ajiunge na ACT-Tanzania ikiwamo kuvutiwa na msingi mama wa chama hicho wa kuweka mbele masilahi ya Taifa.
“Nataka kuwakumbusha wakati napewa uongozi huko nyuma nilishiriki kujenga chama ambacho kina wabunge wanne tu na kuna wakati tukienda kwenye mikutano tunakuta watu 20, lakini tulifikisha hadi wabunge 48.
“Na mimi ni mchapa kazi na sasa nimeamua kuingia kufyeka pori na nitalifyeka pori na tukikutana Novemba tutakuwa na majibu ya maneno yangu…,” alisema Zitto.
Akizitaja sababu tano za kujiunga na ACT-Tanzania alisema katu hatorudi nyumba kupambana kwa ajili ya rasilimali za Taifa na watu wake ikiwa ni pamoja na kuhakikisha nchi inakuwa katika misingi ya uadilifu na uwajibikaji kwa umma.
“Nimekuwa nikipigania uzalendo kwa nchi yangu tangu nilipoanza siasa na nimekuwa nikiweka mbele masilahi ya Taifa dhidi ya kitu kingine chochote,” alisema Zitto.
Sababu ya pili unatokana na chama hicho kuwa pekee kinachokubaliana na itikadi ya ujamaa na kinaamini katika falsafa ya Nyerere iliyo na lengo la kurudisha nchi katika misingi iliyoasisi taifa.
Kutokana na hali hiyo, Zitto alisema anaamini kuwa ACT itasimama katika misingi ya uadilifu na kimeweka miiko na maadili ya viongozi katika kuhakikisha viongozi wa chama hicho wanatakiwa kukubaliana nayo kwa kusaini.
“Katika miaka yangu ya ubunge nimekuwa nikipigania uwajibikaji na uwazi jambo ambalo ninaliamini kwa moyo wangu kwenye utumishi wangu kwa umma.
“Nimefurahi kwamba kati ya misingi 10 ya ACT, uwajibikaji na uwazi ni misingi ambayo naamini inatokana na utumishi wa umma na suala la uwazi limekuwa sehemu ya jina la chama hicho hivyo kwangu ACT ni nyumbani katika siasa na katika utumishi wa umma,” alisema Zitto.
Zitto alisema amejiunga ACT kwa sababu amekubaliana na imani yao ya kujitegemea, bidii, umakini na weledi katika kazi kuwa ndiyo msingi wa maendeleo.
Sababu nyingine aliyotoa ni kukubaliana na imani ya ACT kwamba umoja ni ngao muhimu katika ujenzi wa taifa na Afrika kwa ujumla.
Alisema kwa sababu hiyo ameona upo umuhimu wa kurudisha nchi katika misingi iliyoliasisi taifa.
“Lazima tuirudishe nchi katika heshima ya uongozi wa Bara la Afrika hivyo naahidi kufanya kazi na makundi yote, wanaoamini katika siasa safi na siasa za hoja, tunataka kufungua kurasa mpya wa siasa nchini.
MTANZANIA
WAJUMBE wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali, wamemchagua Mbunge wa Viti Maalumu, Amina Mwidau (CUF) kuwa mwenyekiti wa kamati hiyo.
Katika uchaguzi uliofanyika jana mjini hapa, Mwidau alichaguliwa na wajumbe wa PAC kwa kupata kura 15 dhidi ya mpinzani wake, Lucy Owenya (Chadema) aliyeambulia kura mbili.
Akizungumza baada ya kutangazwa kuwa mshindi wa nafasi hiyo, Mwidau alisema atafanya kazi iliyoachwa na Zitto Kabwe wakati akiiongoza kamati hiyo kwa kuzingatia masilahi ya nchi na siyo watu binafsi.
“Moto ni uleule ambao umeachwa na mwenyekiti mtangulizi wangu, Zitto Kabwe, na tutafanya kazi pale alipoishia maana nikiwa mjumbe wa kamati hii tulifanya kazi kama ndugu wa familia moja.
“Zitto na Deo Filikunjombe waliweka misingi imara katika PAC na hilo tutaendelea nalo na tutafanya kazi kama jicho la Bunge kwa Serikali hasa katika kusimamia na kulinda rasilimali za Watanzania ila tunawaomba waendelee kutuamini,” alisema Mwidau.
Alisema ingawa imebaki takribani miezi minne Bunge kuvunjwa, kamati yake itaendelea na ratiba yake ya mwaka iliyokuwa imepangwa.
“Kama mwenyekiti kazi yangu kubwa ni kuiongoza kamati kwa mujibu wa taratibu, sisi tunakagua hesabu za serikali kuu na mashrika ya umma.
Tunaangalia namna serikali inavyofanya kazi yake, tuna mpango wa kazi, ratiba ya mwaka mzima tutaendelea nayo,” alisema.
Alisema pia kuwa kamati itaendelea na msimamo wa uwajibikaji na uwazi ambao ulikuwa ukisimamiwa na Zitto.
Akizungumzia kuchaguliwa kwa Mwidau kuongoza Kamati hiyo, Mwenyekiti wa zamani wa PAC, Zitto Kabwe alimpongeza kwa kushinda nafasi hiyo akisema ana imani ataendelea kusimamia mifumo ya uwajibikaji.
MTANZANIA
Seriksli imesema imepata hasara ya zaidi ya Sh bilioni nane kutokana na risiti za ununuzi bandia.
Kauli hiyo ilitolewa Dodoma jana na Waziri wa Fedha, Saada Mkuya Salum alipozungumza katika majumuisho ya semina kwa wabunge kuhusu Mfumo wa Malipo nchini.
Mkuya alisema kutokana na mfumo wa kutumia malipo hayo mtu huwasilisha risiti za orodha ya malipo mengi ambayo kwa uhalisia hayapo.
“Ukichukua ile risiti ukienda dukani unakuta hakuna risiti kama hiyo ingawa inakuwapo orodha ya vitu vingi vilivyoainishwa kwamba vitanunuliwa,” alisema Mkuya.
Aliwataka wabunge kuunga mkono Muswada wa Sheria ya mpya ya Mifumo ya Malipo ya Taifa inayotarajiwa kuwasilishwa bungeni leo.
Wabunge wakichangia katika semina hiyo, walitaka sheria hiyo mpya kudhibiti wizi wa fedha kupitia mitandao ya simu.
Mbunge wa Viti Maalum, Martha Mlata (CCM), alisema mbali na sheria hiyo kutungwa sasa, lazima Serikali ibebe mzigo wa wizi kupitia kampuni ya simu, ambao umekwisha kufanyika hadi sasa.
“Watanzania wamekwisha kuibiwa sana kutokana na kufanya miamala mbalimbali kwa kutumia mitandao ya simu.
“Kwa nini jambo hili linalohusu fedha za watu lilianzishwa bila kuaepo sheria na nani ataubeba mzigo wa fedha za watanzania zilizoibwa na makampuni haya,” alisema.
Mbunge wa Chonga, Haroub Mohamed Shamis (CUF) alisema Watanzania wanaibiwa matirioni ya fedha kupitia mitandao ya simu lakini Mamlaka ya Mwasiliano Tanzania (TCRA) imekuwa ikiirushia mpira Benki Kuuya Tanzania (BoT) kwamba ndiyo inatoa leseni za fedha.
“Tanzania kuna takriban kadi za simu milioni 30, kila mtu akiibiwa Sh 100 kwa siku basi tunaibiwa Sh tririoni moja kwa mwaka,” alisema.
Mbunge wa Viti wa Maalum, Diana Chilolo (CCM), alilalamikia huduma za ATM kwamba huduma za VISA na Master Card hazifanyi kazi nje ya nchi.
HABARILEO
RAIS Jakaya Kikwete na Uhuru Kenyatta wa Kenya wameingilia kati mgogoro uliopo baina ya mataifa hayo mawili kuhusu masuala ya usafirishaji na utalii.
 Makubaliano yaliyofanywa na marais hao ni pamoja na Kenya kuruhusu magari ya Tanzania, yanayofanya safari za kupeleka wageni na watalii, maarufu kama ‘Shuttle’ kuingia kupeleka na kuchukua watalii katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Jomo Kenyatta (JKNIA).
 Makubaliano mengine ni kwa Tanzania kupitia Mamlaka ya Usafiri wa Anga (TCAA), kurudisha safari za ndege ya Shirika la Kenya (KQ) kutoka siku 14 za sasa hadi 42 za awali.
 Hayo yameelezwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe wakati akizungumza na waandishi wa habari juu ya kikao kilichowakutanisha marais hao wawili jijini Windhoek, Namibia.
 “Kuanzia saa 10:00 leo hii (jana) magari yote ya Tanzania yana ruksa ya kuingia Kenya kuchukua na kupeleka watalii katika uwanja wa Jomo Kenyatta na ndege za Kenya kuanzia leo zitaruhusiwa kurusha ndege zake kama kawaida kwa siku 42 badala ya 14,” alisema Waziri Membe.
 Aidha, Membe alisema katika kikao hicho, walizungumzia mambo mawili muhimu ambayo ni sekta ya usafirishaji na utalii, ambapo pia walikubaliana ndani ya wiki nne, Mawaziri wa Mambo ya Nje wa nchi hizo waitishe mkutano utakaowajumuisha Mawaziri wa Usafirishaji, Utalii na Maofisa kutoka katika ofisi za Marais.
 Alisema kabla ya kutoa taarifa hiyo, waliwasiliana na Mawaziri wa Uchukuzi na Utalii ambapo pia taarifa hiyo imetangazwa kwa wakati mmoja hapa nchini na Kenya. Waziri Membe alisema mkutano wa kwanza utafanyika mwezi ujao jijini Dar es Salaam, ambapo alisema katika mkutano huo ndipo kiini cha mgogoro huo kitabainika.
“Tanzania na Kenya ni ndugu, ni majirani tusikubali kuchonganishwa wala kuonesha tofauti zetu waziwazi, kama zipo ni vizuri tukaitana na kuzimaliza kimya kimya,” alisema.
Rais Kikwete na Kenyatta wamekutana jijini Windhoek ambako walikwenda kuhudhuria sherehe za miaka 25 ya uhuru wa nchi hiyo na kuapishwa kwa rais wa tatu wa nchi hiyo, Dk Hage Geingob

Comments